Mtandao ni raslimali nzuri kwa watoto ambao huitumia kufanya kazi za shule, kwa burudani na hata kushirikiana na wengine. Hata hivyo, intaneti pia inaweza kuwa mahali hatari pakiwa na hatari kama vile uonevu ama unyanyasaji mtandaoni, ufikiaji rahisi wa maudhui ya ponografia, ulaghai wa mtandaoni, hadaa,  na masuala ya faragha. Kama mzazi, ni muhimu kuchukua hatua ili kuhakikisha kuwa mtoto wako yuko salama mtandaoni. Katika makala hii, tunazungumzia baadhi ya vidokezo vya jinsi ya kufanya hivyo.

 

Je! Watoto wanalengwa vipi mtandaoni?

Watoto wanalengwa kwenye mtandao kwa njia mbalimbali kama vile:

  • Barua pepe za kuhadaa
  • Kubofya viungo vinavyotiliwa shaka kwenye mitandao ya kijamii na michezo ya mtandaoni
  • Kupakua programu ambazo hazijadhibitishwa 
  • Kuzungumza na watu wasiowajua mtandaoni

Hizi hapa vidokezo za njia ambazo tunaweza kutumia kuhakikisha kuwa watoto wako salama mtandaoni:

Vidokezo vya kuwaweka watoto salama mtandaoni

  1. Waelimishe watoto kuhusu usalama mtandaoni: Wafundishe watoto jinsi ya kuepuka uonevu ama unyanyasaji mtandaoni, wavamizi wa mtandaoni na ulaghai. Eleza jinsi ya kutumia mipangilio ya faragha na kuweka maelezo ya kibinafsi salama mtandaoni, na pia jinsi ya kutambua majaribio ya kuhadaa ili kupata maelezo ya kibinafsi na kuwa mwangalifu dhidi ya ulaghai mtandaoni. Unapaswa pia kujaribu kuwasaidia watoto kuelewa hatari za kutoa maelezo mengi ya kibinafsi mtandaoni.
  2. Weka vidhibiti vya wazazi: Tumia vidhibiti vya wazazi ili kuwazuia watoto kufikia tovuti au maudhui yasiyofaa. Hii inaweza kujumuisha kuweka vichujio kwenye injini za utafutaji, kuzuia tovuti mahususi na kudhibiti muda wa kutumia vifaa  kama vile simu ama kompyuta.

    Viungo vifuatavyo vina maelezo ya hatua kwa hatua kuhusu jinsi ya kuweka udhibiti wa wazazi kwenye mifumo tofauti ya mtandao: 

    Facebook: https://screentimelabs.com/parental-controls/facebook-parental-controls/

    TikTok: https://protectyoungeyes.com/apps/tiktok-parental-controls/

    Instagram:https://techcrunch.com/2021/12/07/instagram-announces-plans-for-parental-controls-and-other-safety-features-ahead-of-congressional-hearing/

    YouTube: https://support.google.com/youtubekids/answer/6172308?hl=en

  3. Fuatilia shughuli za mtandaoni za mtoto wako: Angalia kile watoto wanafanya mtandaoni. Angalia wasifu na jumbe zao za mitandao ya kijamii na ufahamu programu na michezo wanayotumia. Unaweza kutumia programu za udhibiti wa wazazi kama vile programu ya Google Family Link kufuatilia shughuli zao mtandaoni.
  4. Himiza umuhimu wa mawasiliano ya wazi: Unda mazingira ambayo watoto wanahisi huru kuzungumza nawe kuhusu uzoefu wao wa mtandaoni. Wahimize kuja kwako ikiwa watakutana na kitu chochote kinachowafanya wasistarehe au waogope. Zaidi ya hayo, waongoze kwenye tovuti fulani muhimu wanazoweza kufikia kwa mahitaji mbalimbali.
  5. Ongoza kwa mfano: Weka mfano mzuri kwa watoto kwa kujizoeza tabia salama mtandaoni wewe mwenyewe. Epuka kutoa zaidi taarifa za kibinafsi mtandaoni na utumie nenosiri dhabiti na uthibitishaji wa vipengele viwili (njia ya usalama ya kudhibiti vitambulisho na ufikiaji ambayo inahitaji njia mbili za kuthibitisha kuwa wewe ni nani kabla ya kutumia jukwaa la mtandaoni). Soma zaidi kuhusu jinsi ya uthibitishaji wa vipengele viwili kwenye mtandao Facebook kwenye kiunga hiki: https://www.facebook.com/help/148233965247823
  6. Weka sheria na mipaka iliyo wazi: Weka sheria wazi za matumizi ya mtandao, kama vile muda unaotumika mtandaoni, tovuti na programu zinazofaa, na aina za maudhui wanazoweza kufikia. Fuatilia shughuli zao za mtandaoni na utekeleze sheria hizi mara kwa mara.
  7. Endelea kujifahamisha: Jifahamishe kuhusu mifumo maarufu ya mitandao ya kijamii, programu na mitindo ya mtandaoni ambayo inaweza kuwa na madhara kwa watoto. Hili litakusaidia kuelewa mifumo ambayo mtoto wako anatumia na kukuruhusu kuwa na mazungumzo ya habari kuhusu matumizi yake ya mtandaoni
  8. Tumia injini za utafutaji zilizoundwa kwa ajili ya watoto: Wahimize watoto kutumia injini za utafutaji zinazofaa watoto kama vile Google Kids Space ambazo huchuja maudhui ya watu wazima na nyenzo nyingine hatari ambazo hawapaswi kuona. Mitambo mingine ya kutafuta ambayo ni sawa kwa watoto ambayo unaweza kutumia ni pamoja na:
  • Kiddle (www.kiddle.co): Kiddle ni injini ya utafutaji iliyoundwa mahsusi kwa ajili ya watoto. Inatumia teknolojia ya utafutaji salama ya Google ili kuchuja maudhui machafu na kuonyesha matokeo ya utafutaji kwa njia inayowafaa watoto. Matokeo ya utafutaji yanajumuisha mchanganyiko wa tovuti salama, picha na video.
  • KidzSearch (www.kidzsearch.com): KidzSearch ni injini ya utafutaji iliyoundwa kwa ajili ya watoto. Inatoa matokeo ya utafutaji yaliyochujwa kutoka vyanzo mbalimbali vinavyoaminika na inajumuisha picha, video na michezo ya elimu. KidzSearch pia inatoa jukwaa salama la wiki liitwalo KidzTube, ambapo watoto wanaweza kupata maudhui yanayolingana na umri wao.
  • Safe Search Kids (www.safesearchkids.com): Safe Search Kids ni injini ya utafutaji inayotumia teknolojia ya Utafutaji Salama ya Google ili kuchuja maudhui machafu. Inatoa mazingira salama kwa watoto kutafuta wavuti na pia wanaweza kutafuta picha na video.
  • KidRex (www.kidrex.org): KidRex ni injini nyingine ya utafutaji inayowafaa watoto ambayo huchuja maudhui yasiyofaa. Inatumia teknolojia ya SafeSearch ya Google ili kuhakikisha kuvinjari kwa usalama kwa watoto. Matokeo ya utafutaji yanawasilishwa katika mtindo wa rangi na kuvutia.
  • Swiggle (www.swiggle.org.uk): Swiggle ni mtambo wa kutafuta unaomfaa mtoto uliotengenezwa na wataalamu wa Usalama Mtandaoni katika Gridi ya Kujifunza ya Kusini Magharibi (SWGfL). Inatoa matokeo ya utafutaji salama na inajumuisha kipengele cha kipekee cha 'WebRover' kinachoruhusu watoto kuchunguza tovuti tofaouti bila kujihatarisha.
  • YouTube Kids (https://www.youtubekids.com): YouTube Kids ni programu ya video na tovuti ya watoto iliyotengenezwa na YouTube. Programu ni toleo la YoutTube winayaolenga watoto pekee, yenye maudhui yaliyoratibiwa vipengele vya udhibiti wa wazazi, na uchujaji wa video zinazochukuliwa kuwa zisizofaa kutazamwa na watoto walio na umri wa chini ya miaka 13.

Vidokezo/mwongozo kwa watoto ikiwa wakikabiliwa na shughuli zozote za mtandaoni wasioamini ama wanazoshuku:

  1. Mwambie mtu mzima unayemwamini mara moja kuhusu tabia unazoshuku au isiyofurahisha au ikiwa mtu mtandaoni akitaka kujua taarifa zako za kibinafsi kama vile jina lako kamili, anwani, nambari ya simu au maelezo ya shule unaposoma.
  2. Mwambie mtu mzima unayemwamini au watu wanaofaa ambao wanaweza kukusaidia kufanya maamuzi ikiwa utaona au kusikia picha, video, au ujumbe zinazokufanya ukose raha ukiwa mtoto- hilo linaweza kuwa jambo zito.
  3. Mwambie mtu mzima unayemwamini ikiwa unalengwa mtandaoni, au unanyanyaswa kupitia vitisho au matusi kupitia ujumbe, maoni au machapisho kwenye mitandao ya kijamii. Wanaweza kukupa mawaidha na kuchukua hatua zinazofaa kushughulikia suala hilo.
  4. Ikiwa mtu mtandaoni atajaribu kuanzisha uhusiano wa karibu nawe, mara nyingi kwa nia ya kukudhulumu au kukudanganya, ni muhimu kuripoti. Mifano ni pamoja na mtu mzima anayetaka kufanya mazungumzo ya faragha nawe, kukuuliza umtumie picha zako au kukutumia uchi wao, kufanya ushawishi usiofaa au kujaribu kukutana nawe ana kwa ana.
  5. Kuwa mwangalifu unapobofya viungo au kupakua viambatisho na programu, kwani zinaweza kuwa na virusi au maudhui mengine hatari.

 

Rasilimali za ziada:

 

 

Mahali pa kuripoti unyanyasaji wa mtandaoni:

 

Nambari za Usaidizi za Kitaifa

  1. Simu: 116/ / 0732 263 554. 
  2. WhatsApp: +254 722 116 116.  
  3. Barua pepe: 116@childlinekenya.co.ke

Nambari ya usaidizi ya shirika la Terres Des Hommes (TdH) katika kambi ya  Dadaab: 0800720648 

 

Tazama huduma za watoto zinazotolewa na TDH katika IFO 2 HAPA 

Ikiwa una maswali yoyote, tafadhali tuandikie kupitia ukurasa wa Facebook wa Julisha.Info au zungumza nasi kupitia WhatsApp (+254110601820) ,Jumatatu hadi Ijumaa kutoka 08:00 asubuhi hadi 5:00 jioni